Friday, November 27, 2015

JE SILAHA ZAKO ZINA UWEZO?

NENO LA LEO - JE SILAHA ZAKO ZINA UWEZO?
Tafakari: 2Wakorintho 10:3-5
"Maana ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili; maana Silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina UWEZO KATIKA MUNGU hata kuangusha Ngome; tukiangusha Mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila FIKIRA ipate KUMTII Kristo".
Nakumbuka usemi wa marehemu Baba wa Taifa Mwalimu JK Nyerere, wakati Raisi wa Uganda Idd Amini alipoivamia Tanzania, Baba wa Taifa alisema "Nia tunayo, Sababu tunayo na Uwezo wa kumpiga tunao". Ndipo akatoa Amri ya Kumpiga na Kuivunjilia mbali ngome yake katika nchi yake.
Katika ulimwengu wetu huu uliotekwa na Adui shetani, ni jambo la kawaida kusikia Watu wanajiita ni Wakristo, wengine wanajiita wacha Mungu, wengine wameokoka n.k. Wanauwezo mkubwa hata wa kuimba nyimbo za dini kwa hisia kubwa, lakini jambo la kushangaza, asilimia kubwa unawakuta bado ni watumwa wa yule Adui.
Mbali na kuonekana watu wema au wacha Mungu machoni pa watu, ndani ya Mawazo yao au Fikira zao, kumejaa Visasi, Uadui, Kutosamehe, Husuda, Wivu. Wakati mawazo, maneno na matendo ya Ngono na Mapenzi yakiendelea kukamata akili za Vijana kwa Wazee, wakipigwa upofu wasione kuwa ni dhambi; Mungu anazidi kutoa wito wa Kushinda vita.
Wapendwa Ngome kuu za Shetani ziko katika MAWAZO au FIKIRA, huko ndiko zinatakiwa zivunjiliwe mbali, hatimaye mawazo yetu yaunganishwe na Kristo. Hayo yanawezekana tu kwa watu ambao wameruhusu utawala wa Ufalme wa Mungu kuwa ndani yao, kwa njia ya Roho mtakatifu.
Ni wakati wa kila mmoja kujipima, kuwa je; ni kweli amezivaa Silaha zenye Uwezo wa Mungu? Mawazo na Fikira Je zinapatana na Mungu au zimejaa Uchafu wa yule Adui shetani? Yesu Kristo alikuja kwa ajili ya kutuokoa kutoka katika mateka ya dhambi, na huu ndio uhuru wa Kweli.
NAWATAKIA WOTE SIKU NJEMA YENYE BARAKA TELE NA MAFANIKIO KATIKA MWILI NA ROHO.

Tuesday, November 17, 2015

Mwanamke wa Ufunuo 17 ni Kanisa la Rumi

Mwanamke wa Ufunuo 17 ni Kanisa la Rumi



    TUWEKE kumbukumbu zetu makini zaidi.
 Feburuari 26 mwaka 2009,William Shao aliandika katika Gazeti la Rai,kwamba mwanamke anayefanana na Yule wa Ufunuo wa Yohana 17:3-11, amejemgewa sanamu mbele ya Jengo la Bunge la Umoja wa Ulaya, huko Brussels,Ubelgiji.
Shao, alienda mbali zaidi kusema, hata jingo lenyewe la Bunge la Ulaya(EU) mjini Brussels, halina tofauti sana taswira yake na Mnara wa Babeli.

Shao, anasema sanamu ya mwanmke aliyeketi juu ya mnyama mbele ya ofisi za Bunge la Ulaya, haikuwekwa kwa bahati mbaya; inatafsiri jambo fulani muhimu wewe kuelewa.                     

 Ulaya, ilikuwa himaya ya Dola ya Rumi; na Mwanamke huyo wa mjini Brussels anayeitwa, “Europa Goddes” ni mungu mke wa Ulaya.
 Naam, mungu jike wa Ulaya ndiye mtawala wa Ulaya na makoloni yake duniani, na mji anaoketi huitwa kwa Jina la Siri, “Babeli” Ufunuo 17:5!!
Umeona picha ya mnara wa Babeli? Ni kama alivyosema mwandishi William Shao,kwamba inafanana sana na jingo la Bunge huko la Ulaya huko mjini Brussels, Ubelgiji.
‘Uropa Goddes’-mungu jike wa Ulaya,hufananishwa na jiji la kale sana Babeli ambayo ni Irak ya siku hizi.
 Kulingana na Biblia, mwanamke katika Unabii ni kundi la waabuduo-kanisa, waumini. Kuna wanawake wawili katika Ufunuo wa Yohana, Ufunuo 12 na 17; moja huwakilisha kundi nyoofu katika maadili ya kidini na, mwanamke wa Ufunuo 17 ni kundi kengeufu linalojichanganya na waabudu sanamu, anasa za dunia na uchafu wa kiroho.
Katika Hosea 2:10,Yeremia 3:14 na 2Korintho 11:2 uhusiano baina ya Mungu Mwenyezi na Kanisa lake hufananishwa na uhusiano wa ndoa,kati ya mume na mke.
Katika Ufunuo 21:2 mji wa Yerusalem umefananishwa na ‘Bibi Harusi’ yaani mwanamke safi. Kanisa la Mungu linapoungana na dunia na anasa na kuabudu sanamu, hufananishwa na UZINZI(Tazama Yakobo 4:4).
Naam, Yakobo anawaita watu wa Mungu waliomwacha na kuungana na Dunia ya dhambi kwamba ni Wazinzi, waasherati, makahaba!
 Ni hapa, tunapomaizi kwamba mwanamke wa Ufunuo 17:3 ambaye ni “mungu-jike wa Ulaya” ni Kanisa la Mungu lililoungana na Dunia na mivuto yake na anasa zake na kumwacha Mungu.
Anasa,ulevi,falsafa,ibada ya sanamu na miungu,ushoga,ulawiti hata wa watoto chekechea n.k
Mavazi ya ‘Mwanamke’ huyo ni rangi nyekundu na zambarau, ambayo yalivaliwa na makuhani wa miungu huko Babeli ya kale.
 Hawa ni kundi tajiri wenye madini,vito vya thamani na urembo ambalo linamvuto mkubwa kwa Wafalme wa Dunia. Kanisa hilo linasemwa kutawala miongoni mwa wafalme wa dunia(Marais, Mawaziri Wakuu,Wafalme n.k) yaani hubebwa na watawala wa Umoja wa Ulaya huko mjini Brussels(Tazama Ufunuo wa Yohana 17:4-6).
Muungano haramu wa Kanisa la Mungu na viongozi wa dunia(uzinzi) ndiyo kuungana kufanya yaliyo kinyume na Amri 10 za Mungu. Kuungana na upagani, kuabudu sanamu na miungu kama jua, sayari,nyota na mwezi.
Mwanamke wa mjini Brussels anao watoto wake nao ni ‘Makahaba’ yaani wazinzi wa kiroho.
Sasa, tutazame kwa makini; kama mji wa Brussels mwaka 96 AD wakati Mtume Yohana anaandika kitabu cha Ufunuo,ulikuwepo? Hasha!!
 Nchi nzima ya Ubelgiji ina watu wasiozidi milioni 12. Brussels siku hizi una wakazi milioni 1.5 tu.
Tuutafute mji wa kale sana Ulaya, ambao Yohana aliuita jina la mafumbo Babeli. Umejengwa juu ya milima saba(ufunuo 17:9).
 Mwaka 753 BC mji uliojengwa Ulaya ni Rome. Hata London haukuwepo, Uingereza ilikuwa kijiji kidogo mwaka 1000 AD. Hata mwaka 500 BC Rome lilikuwa jiji tena “SUPER POWER” Duniani, ulijengwa na Romulus.
 Katika mji huu ndiko yaliko mamlaka ya kidini,Vatican. Unaposema Vatican unasema kanisa la Mungu. Vatican imekuwa nchi Feburuari 11, mwaka 1929 zama za Benito Mussolini.
Rome ni mahali ambapo wameishi ma-Baba Watakatifu(Popes) wa Katoliki wapatao 302. Mji huu ulikuwa makao makuu ya dola ya Rumi, hata zama za Yesu,mitume na zama za Biblia Takatifu yaani kati ya mwaka BC 1500 ZAMA ZA MUSA Hadi 96 AD alipofariki Yohana wa Patmo.
 Nataka msomaji atambue kwamba, waandishi wa Biblia waliposema Babeli,baada ya kuanguka kwa mji wa Babeli, walimaanisha MJI WA ROME(Isaya 21:9).
Fahari yake na ulikuwa mji mkuu wa biashara duniani. Kanisa Katoliki linadai Petro aliyefika mjini Rome mwaka 42 AD na akauliwa na Kaisari Nero Mkatili, mwaka AD 67,ndiye Papa wa Kwanza kwa Kanisa hilo.
 Tuwatazame mapapa. Huchaguliwa na Makadinari kama 131 hivi. Papa Benedict XVI yeye alichaguliwa na Makadinali 117, ambao hawakuwa na umri wa miaka 80. Papa ni Mwakilishi wa Yesu,mrithi wa Mtume Petro,Mkuu wa Mitume wote duniani,Papa ni Mamlaka na nguvu-Tazama Danieli 7:25.
 Rome, ni mahali Kanisa la Mt.Petro lilipojengwa juu ya Kanisa la Petro; linaitwa, St.Peter’s Basilica. Limejengwa KATIKA ENEO LA EKARI SITA.
Hili kanisa, St. Peter’s Basilica, lina urefu wa futi 700 na upana ni futi 450 na linaweza kuchukua watu 80,000 kwa wakati mmoja.
Rome ni jiji lililopo nyuzi sawa na New York kwa nyuzi za Latitude; ni jiji lenye Coliseum, ambamo yalifugwa masimba yaliyorarua Wakristo maelfu.
Rome,uko futi 40 hadi 270 juu ya usawa wa Bahari. Jiji lenye kelele nyingi kuliko mji wowote duniani,lipo kando ya Bahari ya Mediterranean.
 Zama za Papa Pius XII alibebwa kwenye kiti cha enzi kiitwacho, Sedia Gastatoria ambacho ni kiti cha enzi cha dhahabu chenye rangi nyekundu.Papa huketi hapa mara anapochaguliwa na Moshi  Mweupe, hutoa BARAKA Duniani- Urbi et Orbi.
Rome umejengwa juu ya milima saba: CAPITALINE, PALATINE, AVENTINE, QUIRINAL, VIMINAL, ESQUILINE, na CAELIAN.
Hapa, ndipo liketipo kanisa lile la Mungu ambalo sasa linataka kugeuka kuwa kama Yule mama wa mjini Brussels.
Mwanamke huyu ni kanisa. Kanisa linapoungana na dunia na kuacha usafi wa kiroho huitwa, ‘BABELI’ ya siri iliyoanguka na Mungu huwaita watu wake watoke humo(Ufunuo 18:2-4).
Kuanguka ni kuacha usafi wa kiroho,kumwacha Mungu na kuungana na uchafu kama unajisi,siasa za kugombea tawala za dunia,ufisadi,mapinduzi,ulawiti,ushoga n.k
Jiji lenye utajiri wa dhahabu na vito vya thamani lenye kuwakosesha watu kwa mafundisho yenye kuridhia dhambi(uasi wa sheria ya Mungu) kama jambo dogo tu-Uhuru na demokrasia,haki za binadamu n.k
Wapo wanaofuata kila jambo na ni ‘watoto’ wa Yule mama wa mjini Brussels. Tafakarini.

JE! NAWEZA KULIPATA KANISA LA MUNGU LEO?

JE! NAWEZA KULIPATA KANISA
LA MUNGU LEO?
Mara kwa mara Mungu ametoa ujumbe wa pekee kukidhi mahitaji ya vizazi tofauti mbali mbali: ujumbe wa kumsaidia Adamu na Hawa baada ya dhambi kuiharibu dunia yao, ujumbe kwa ulimwengu uliokuwako kabla ya gharika ile kuu ya maji, ujumbe kwa Israeli wakati Ashuru au Babeli ilipowatishia. Yesu alikuja na ujumbe maalum kwa siku zetu. Sura ya 12 na 14 ya Ufunuo hutoa muhtasari wa ujumbe wa Mungu wa pekee kwa ajili yetu leo. Katika GUNDUA Mwongozo huu na mwongozo ule unaofuata, tutauangalia ujumbe huo.
1. Kanisa Lilianzishwa Na Yesu
Maisha na mafundisho ya Yesu yalianzisha umoja wa imani na ushirika wa karibu sana katika kanisa lile la mitume walilolianzisha. Mitume wale walikuwa na uhusiano wa karibu kabisa na Kristo yule aliyefufuka. Paulo alitoa picha ya kifungo hicho cha karibu sana na kukilinganisha na uhusiano wa ndoa:
"Naliwaposea Mume mmoja, yaani, Kristo, ili niwalete ninyi kwake mkiwa bikira safi." - 2 Wakorintho 11:2.
Kulingana na maneno ya Paulo, kanisa la Kikrsto ni mwanamke safi, ni bibi-arusi wa Kristo, ishara inayofaa kabisa kwa kanisa lake Kristo alipendalo. Katika Agano la Kale mithali iyo hiyo inatumika kuielezea Israeli, yaani, wateule wa Mungu. Mungu aliwaambia Israeli: "wewe kama bibi-arusi ulinipenda mimi" (Yeremia 2:2); "Mimi ni mume wenu" (Yeremia 3:14).
Kitabu cha Ufunuo pia kinazungumza juu ya kanisa kama mwanamke:
"Ishara kuu na ya ajabu ilionekana mbinguni: mwanamke aliyevikwa jua, na mwezi ulikuwa chini ya miguu yake, na taji ya nyota kumi na mbili juu ya kichwa chake" - (Ufunuo 12:1).
Mwanamke huyo ame"vikwa jua". Maneno hayo yanadokeza kanisa linalong'aa kama jua, kwa sababu ya kuvikwa utukufu wa kuwako kwake Kristo. Yesu, "Nuru ya Ulimwengu" (Yohana 8:12), anaangaza kupitia kwa washiriki wa kanisa lake, nao kwa upande wao wanapaswa kuwa "nuru ya ulimwengu" (Mathayo 5:14).
Mwanamke huyo ana"mwezi chini ya miguu yake." Mwezi huo unawakilisha nuru ya Injili iliyoakisiwa [iliyoangaza] katika dhabihu na taratibu za ibada ya watu wa Mungu katika Agano la Kale. Mwezi huo ukiwa "chini ya miguu yake" unadokeza kwamba nuru ya Injili iliyoakisiwa imepitwa na huduma anayofanya Kristo.
Mwanamke huyo anayo "taji ya nyota kumi na mbili juu ya kichwa chake." Nyota zinawakilisha vizuri sana mitume wale kumi na wawili, watu waadilifu ambao ushuhuda wao juu ya Yesu unang'aa sana mpaka siku hii ya leo.
Ni dhahiri, basi, kwamba maelezo yamhusuyo mwanamke huyo yanaonyesha kwamba Yohana katika mawazo yake analiona badiliko lililotokea kutoka kwa watu wa Mungu, Israeli, katika Agano la Kale kwenda kwenye kanisa lile la Kikrsto la Agano Jipya alilolianzisha Yesu. Jua, mwezi, na nyota huitilia mkazo huduma ya kupeleka nuru inayofanywa na kanisa hilo la Kikristo kwa kuzitangaza hizo Habari Njema.
2. Matukio Yanayofuatana Ya Kushindwa Kwa Shetani
Kuingia kwa mwanamke huyo kunaweka jukwaa kwa matukio haya makuu yanayofuatana:
"Alikuwa mja mzito, naye akapaaza sauti kwa maumivu na uchungu wa kujifungua mtoto. Kisha, ishara nyingine ikatokea mbinguni: joka mkubwa jekundu na lenye pembe kumi na vichwa saba; na kila kichwa kilikuwa na taji. Joka hilo liliburuta kwa mkia wake theluthi moja ya nyota za anga na kuzitupa duniani. Nalo lilisimamaa mbele ya huyo mama aliyekuwa karibu kujifungua mtoto, tayari kabisa kummeza mtoto, mara tu atakapozaliwa. Kisha, mama huyo akajifungua mtoto wa kiume ambaye atayatawala mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Lakini mtoto akanyakuliwa na kupelekwa kwa Mungu na kwenye kiti chake cha enzi" - Ufunuo 12:2-5.
Wakuu watatu wanashiriki katika mfululizo wa matukio haya:
Mwanamke, huyo tayari ametambulishwa kama kanisa lake Mungu.
Mtoto wa kiume aliyezaliwa na mwanamke huyo ana"nyakuliwa hata kwa Mungu na kwenye kiti chake cha enzi," na siku moja "atayatawala mataifa yote." Yesu ndiye mtoto peke yake aliyepata kuzaliwa katika ulimwengu huu ambaye alinyakuliwa kwenda kwenye kiti cha enzi cha Mungu na ambaye siku moja atayatawala mataifa yote.
Joka anamwakilisha Ibilisi, au Shetani.
"Kisha kukazukaa vita mbinguni: Mikaeli na malaika wake walipigana na hilo joka, nalo likawashambulia pamoja na malaika wake. Lakini joka hilo na malaika wake walishindwa, na hatimaye hapakuwa tena na nafasi mbinguni kwa ajili yao. Basi, joka hilo kuu likatupwa nje. Joka hilo ndiye yule nyoka wa kale ambaye huudanganya ulimwengu wote. Naam, alitupwa duniani, na malaika wake wote pamoja naye." - Ufunuo 12:7-9.
Picha hiyo inakuwa dhahiri mara tu tunapoifahamu mifano hiyo. Ibilisi na malaika zake "wa[lipo] poteza mahali pao mbinguni," wali"tupwa duniani." Yesu alipozaliwa katika dunia hii, Ibilisi alijaribu kumwua Yesu, mwana yule wa kiume, mara tu alipokwisha kuzaliwa. Alishindwa, kisha Yesu "akanyakuliwa" kwenda kwenye kiti cha enzi cha Mungu.
Ndipo Shetani akaondoka kwenda kuliangamiza kabisa kanisa la Kristo alilolianzisha Kristo. Mtume Yohana, aliyekiandika kitabu cha Ufunuo, aliliona kidogo tu pambano hilo kuu kati ya Kristo na Shetani likipiganwa vikali sana juu ya dunia hii. Vita hiyo ilipofikia kilele chake wakati ule wa kusulibiwa kwake Kristo, Yohana alisikia sauti ikipiga kelele kutoka mbinguni, ikisema:
"Kisha nikasikia sauti kubwa kutoka mbinguni ikisema: Sasa umefikia mkombozi na nguvu na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake! Maana yule aliyewashtaki ndugu zetu mbele ya Mungu ametupwa chini. Naam, ametupwa chini huyo anayewashtaki usiku na mchana"- Ufunuo 12:10. (Linganisha na Yohana 12:31 na Luka 10:18).
Yesu alipata ushindi dhidi ya Shetani pale msalabani. Wakati ule ndipo alipothibitisha uhakika wa mpango ule wa "wokovu" na kutoa "uwezo" wa kuzipinga hila za Shetani. "Ufalme wa Mungu" ukaimarishwa, na "mamlaka" ya Mwokozi ya kuwa Kuhani wetu Mkuu na Mfalme wetu ikawa imethibitishwa.
"Sasa umekuja wokovu" ni tangazo linaloonyesha kwamba tendo lile la kilele la historia limefika. Kuzaliwa kwake Kristo, Mwokozi wa ulimwengu, kumekwisha kutokea (fungu la 5). Licha ya majaribu makali ya Shetani, Yesu aliishi maisha yasiyo na dhambi, alikufa na kufufuka akiwa mshindi dhidi ya dhambi na mauti (fungu la 10). Shetani ameshindwa milele (fungu la 7-9). Msalaba umetukuzwa katika uwezo wake wote.
Tangazo hili, "Sasa umekuja wokovu," halimpendezi Yohana tu, bali malimwengu yote:
"Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, na ninyi mkaao humo! Ole kwa nchi na bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kuja kwenu! Amejaa ghadhabu nyingi, kwa sababu anajua kwamba ana wakati mchache tu." - (Ufunuo 12:12).
Mbingu yote ilisherehekea ushindi wa Kristo. Kristo aliyavunjilia mbali madai ya aina yo yote ile aliyokuwa nayo Shetani zamani kuhusu kuwa na mahali pake kule mbinguni, na yule Shetani aliyeshindwa akapoteza milele madai yake aliyosema dunia hii ni yake.
3. Kanisa La Kikristo Katika Mapambano Dhidi Ya Shetani
Kabla Yesu hajapaa kwenda mbinguni alilianzisha kanisa la Kikristo (ambalo linafananishwa na mwanamke). Kifo chake pale msalabani kililipa hilo kanisa la Kikristo uwezo wa kumshinda Shetani.
"Nao [Kanisa la Kikristo] wakamshinda [Shetani] kwa damu ya Mwana-Kondoo na kwa neno la ushuhuda wao; hawakuyapenda sana maisha yao kiasi cha kuogopa kufa." - (Ufunuo 12:11).
Kristo anaweza kulipa kanisa lake uwezo wake sasa, yaani, kulipa lile tunda la ushindi wake. Yesu alimshinda Shetani kabisa kwa njia ya kanisa lake. Sifa tatu zinalitambulisha kanisa hilo lenye kushinda katika karne zilizokuwa zikiendelea kupita za kipindi hiki cha Kikristo:
"Wakamshinda [Shetani] kwa damu ya Mwana-Kondoo." Yesu alinyakuliwa hadi kwenye kiti cha enzi cha Mungu ili apate kuifanya damu yake iwe na matokeo mema katika maisha ya wafuasi wake. Yeye anaweza kuiondoa kumbukumbu ya dhambi zetu, anaweza kutuokoa kwa njia ya damu yake iliyomwagika (1Yohana 1:7), na kutupa uwezo wa kuishi maisha yenye afya ya Kikristo siku kwa siku.
"Hawakuyapenda sana maisha yao kiasi cha kuogopa kufa." "Damu ya Mwana-Kondoo" iliwafanya wawe tayari kufa kwa ajili ya kazi yake Kristo; hawa"kuogopa kufa." Mungu alikuwa ameteseka sana,kwa hivyo Wakristo wale wafia dini walikuwa tayari kuteswa na kuuawa. Hata watoto wadogo walijitoa mhanga hatimaye. Kisa kinasimuliwa cha mama mmoja Mkristo aliyetupwa kwa Simba katika uwanja wa michezo wa Kiroma kwa kuwa alitoa utii wake kwa Kristo, wala si kwa serikali. Binti yake mdogo,
badala ya kujikunyata kwa hofu kuu, alisikia ari ya kujitoa wakfu ikijaa ndani yake. Wale simba walipomshambulia mama yake, alisimama na kupiga kelele, "Mimi pia ni Mkristo." Maafisa wa Kiroma wakamkamata na kumtupa kwa nguvu kwa wanyama wale wenye njaa.
"Wakamshinda [Shetani]… kwa neno la ushuhuda wao." Sio maneno, bali neno la ushuhuda wao yaani, ushuhuda wa maisha yao, ushuhuda wao hai kwa uweza wa Yesu na injili yake. Katika zile saa za giza nene kabisa la kipindi kile cha Kikristo, jeshi la Wakristo - kuanzia kwa mababa wale wa kwanza wa kanisa hadi kwa wanamatengenezo wa kanisa la Kiprotestanti - waliyashinda mambo yote mabaya mno, ambayo Ibilisi aliweza kuwatupia kwa nguvu, kwa njia ya ushuhuda wao tu wenye nguvu wa maisha yao.
Ufunuo 12:11 huonyesha picha ya kanisa linaloshinda ambalo limejaa washindi: mitume, wafia dini, wanamatengenezo ya kanisa, na Wakristo wengineo waaminifu. Upole, uaminifu, ujasiri, na ushindi wao umenguruma kushuka katika karne nyingi na kuupindua ulimwengu.
Kwa kuwa Shetani alishindwa kumwangamiza Yesu alipoishi hapa duniani, sasa anajitahidi sana kumwangamiza Kristo anayeishi ndani ya kanisa lake.
"Joka lilipotambua kwamba limetupwa chini duniani, likaanza kumwinda yule mama aliyekuwa amejifungua mtoto wa kiume. Lakini mama huyo akapewa mabawa mawili ya tai apate kuruka mbali sana na hilo joka, mpaka mahali pake jangwani ambapo angehifadhiwa salama kwa muda wa miaka mitatu na nusu. Basi, joka likatapika maji mengi kama mto, yakamfuata huyo mama nyuma ili yamchukue. Lakini nchi ikamsaidia huyo mama: ikajifunua kama mdomo na kuyamezaaa maji hayo yaliyotoka kinywani mwa hilo joka - (Ufunuo 12:13-16).
Kama vile ilivyotabiriwa, katika zama zile za giza za kipindi kile cha Kikristo, Shetani alitoa "mto" wa mateso ili kufanya kanisa li"chukuliwe na mkondo ule wa mto." Shetani anataka kuufutilia mbali mvuto wa Kristo kwa kulifutilia mbali kanisa lake, tena anatumia kila hila ambayo akili yake nyingi iliyojaa uovu inaweza kubuni. Kimsingi Joka anamwakilisha Shetani. Lakini kumbuka kwamba Shetani anazitumia taasisi za wanadamu katika utendaji wake kama joka ili kuwashambulia watu wa Mungu. Alimtumia mfalme wa Kiroma Herode katika jaribio lake la kumwua mtoto Kristo mara tu alipokwisha kuzaliwa. Alifanya kazi yake kupitia kwa viongozi wa dini wenye husuda na wenye kuwania madaraka waliomnyemelea na kumsumbua Mwokozi, na hatimaye kumwua juu ya ule msalaba. Lakini ule ulionekana kama ni ushindi mkubwa usio na kifani wa Kristo.
Akiwa amekasirika vibaya sana dhidi ya kushindwa kwake pale msalabani, Shetani akaielekeza ghadhabu yake dhidi ya Kanisa lile alilolianzisha Yesu. Katika miongo [miaka kumi-kumi] iliyofuata baada ya kusulibiwa kwake Kristo, maelfu waliuawa katika ule uwanja wa duara uliojengwa mjini Roma (Colosseum), maeneo tupu ya pembe mraba yaliyokuwa mijini, magereza yale ya chini ya ardhi, na katika maficho ya jangwani.
Mwanzoni wale wenye mamlaka [serikali] ya kidunia walianzisha hayo mateso. Lakini baada ya kufa wale mitume badiliko lilitokea taratibu ndani ya kanisa lile. Katika kipindi kile cha karne ya pili, ya tatu, na ya nne, wengi ndani ya kanisa lile walianza kuzibadili kidogo zile kweli zilizokuwa zimefundishwa na Kristo pamoja na mitume wake. Viongozi fulani, walioasi hata wakaanza kuwatesa Wakristo wale waliosisitiza kuwa na usafi wa itikadi [imani] za Agano Jipya.
Wataalam wa Biblia wanakadiria kwamba takriban milioni 50 ya wale waliokuwa waaminifu waliuawa. Katika jitihada yake ya kulizamisha na kuliangamiza kanisa, Ibilisi alitoa "mto" wa mateso ili kulifanya "lichukuliwe [lile kanisa] na mkondo ule wa mto." "Lakini nchi ikamsaidia yule mwanamke kwa… kuumeza ule mto" wa mateso na mafundisho ya uongo.
Katika kipindi cha mateso ya Zama za Kati [1100-1500], kanisa la kweli lilijiondoa kutoka katika uongozi ule ulioasi na kujificha "Nyikani, mahali alipoandaliwa na Mungu, ili wamlishe muda wa siku 1,260" (fungu la 6). Utabiri huo ulitimizwa katika kipindi cha miaka 1260 ya mateso kuanzia mwaka wa 538 hadi mwaka wa 1798 B.K. (siku moja mara nyingi husimama badala ya mwaka mmoja katika unabii wa mifano wa Biblia, angalia Ezekieli 4:6).
Katika kipindi cha karne za giza Wakristo waaminifu walioiamini Biblia walipata kimbilio lao po pote walipoweza kupapata kwa mfano, katika mabonde ya Wawaldensia wa Italia magharibi na Ufaransa mashariki, na katika kanisa la Kikeltiki [Waskoti Waairishi, Waweishi] la visiwa vya Uingereza.
4. Kanisa La Mungu Katika Siku Hizi Zetu
Jambo hilo linatufikisha katika siku hizi zetu - yaani, kwenye kanisa la kweli la Kristo tangu mwaka wa 1798. Kama ambavyo ingeweza kutarajiwa, yule joka bado amewakasirikia watu wa Mungu. Vita kuu isiyoonekana kwa macho inaendelea. Kwa kweli, Shetani anafanya shambulio lake kubwa kabisa dhidi ya kanisa hilo muda mfupi tu kabla ya kuja kwake Yesu.
"Ndipo yule Joka [Ibilisi] akamkasirikia sana yule mwanamke [Kanisa la Mungu], akaenda zake afanye vita dhidi ya wazao wake waliosalia - wale wanaozitii amri za Mungu na kuwa na ushuhuda wa Yesu." - (Ufunuo 12:17).
Unabii huu unalenga katika siku zetu hizi. Shetani amekasirika sana; anafanya vita dhidi ya wazao wa mwanamke waliosalia" - yaani, dhidi ya watu wa Mungu wa siku hizi. Angalia alama zao zinazowatambulisha:
(1)Waumini hao wa siku za mwisho wanao "ushuhuda wa Yesu." Kwa uaminifu wakiyang'ang'ania mafundisho safi ya Neno la Mungu, wanamshuhudia Yesu kwa njia ya maisha yao yenye nguvu nyingi ya Kikristo.
(2) Wakristo hao wa siku za mwisho ni watu wa unabii. Kuupokea ule "ushuhuda wa Yesu Kristo" kulimwezesha Yohana kukiandika kitabu kile cha Ufunuo (Ufunuo 1:1-3). Kundi hilo la mwisho la waumini linapokea karama ile ile: yaani, ushuhuda wa moja kwa moja toka kwa Mungu kupitia kwa mjumbe wa kibinadamu. Karama yao ya unabii inalenga juu ya ufunuo wa Mungu kuhusu utume wao na mwisho wao.
(3) Wakristo hao wa siku hizi za mwisho wanatambulikana pia kama "wale wanaozitii Amri [kumi] za Mungu." Hawatetei tu ukamilifu wa hizo Amri Kumi, bali wanazitii pia. Upendo wa Mugu ulio mioyoni mwao unawaletea utii unaotolewa kwa moyo wa furaha (Warumi 5:5; 13:8-10).
Wakristo hao wa siku hizi za mwisho wanakifuata kielelezo cha Kristo na cha kanisa lile la kwanza kwa kuzitii amri [kumi] za Mungu. Jambo hilo linamkasirisha vibaya sana yule Joka - yaani, yule Ibilisi. Naye anapigana vita dhidi ya "wazao" wa mwanamke "waliosalia" kwa sababu wanatoa ushuhuda kwamba upendo wao kwa Mungu unawafanya wafuasi wake hao kuwa watii. Kama vile Kristo alivyoagiza, aliposema:
"Mkinipenda, mtazishika amri zangu" - Yohana 14:15.
Maisha ya Wakristo hao wa siku hizi za mwisho yanaonyesha kwamba uwezekano upo wa kumpenda Mungu kwa mioyo yetu yote na kuwapenda wenzetu kama sisi tunavyojipenda wenyewe. Kulingana na maneno ya Yesu, sifa hizo za tabia, yaani, upendo kwa Mungu na upendo kwa watu, hufanya muhtasari wa Amri kumi za Mungu (Mathayo 22:35-40).
Ya nne katika hizo amri inatutaka sisi kuitunza Jumamosi, siku ya saba ya juma, kama Sabato. Kwa kuwa upendo wao kwa Yesu umezitia ndani ya mioyo yao amri zote kumi [Ebr. 8:10; Kut. 20:3-17; Yak. 2:10-12], basi, Wakristo hao wa siku hizi za mwisho ni Wasabato.
Sabato ndicho kiini cha ujumbe wa mwisho wa Mungu kwa watu wake katika kitabu cha Ufunuo, sura ya 12 na 14:6-15. Nguvu zote za mbinguni zinajipanga nyuma ya Wakristo hao wa siku hizi za mwisho walioelezwa katika sura hizo. Mwokozi wao aliye hai ndiye rafiki yao daima, na Roho Mtakatifu anafanya kazi yake "kuwafanya imara kwa nguvu katika utu wao wa ndani." Ahadi yake ni ya hakika. WATAmshinda Shetani "kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao" (Ufunuo 12:11).
Je! unataka kuwa mmoja wa Wakristo hao wa siku hizi za mwisho ambao "wanazitii amri [kumi] za Mungu" tena wa"na ushuhuda wa Yesu"? Kwa nini usikate shauri sasa hivi?

Wednesday, March 11, 2015

JE! NAWEZA KUWA SEHEMU YA KANISA LA MUNGU LEO?sehemu ya kwanza.

Kanisa ni muunganiko wa binadamu wanaomwabudu Mungu katika Roho na Kweli ulimwenguni kote.

Mara kwa mara Mungu ametoa ujumbe wa pekee kukidhi mahitaji ya vizazi tofauti mbalimbali: Ujumbe wa kumsaidia Adamu na Eva baada ya dhambi kuiharibu dunia yao walipojiona uchi, Ujumbe kwa ulimwengu uliokuwako kabla ya gharika ile kuu ya maji, Ujumbe kwa miji ya Sodoma na Gomora kabla ya kuangamizwa kwa moto, Ujumbe kwa Israel wakati Ashuru au Babeli ilipowatishia n.k. Yesu alikuja na ujumbe maalum kwa siku zetu.
Sura ya 12 na 14 ya Ufunuo hutoa muhtasari wa ujumbe wa Mungu wa pekee kwa ajili yetu leo. Tutauangalia ujumbe huo ili tuzingatie sifa zinazotufanya kuwa sehemu ya Kanisa la Kristo leo.
.Kanisa Lilianzishwa Na Yesu
  Maisha na mafundisho ya Yesu yalianzisha umoja wa imani na ushirika wa karibu sana katika kanisa lile la mitume walilolianzisha.Mitume wale walikuwa na uhusiano wa karibu kabisa na Kristo yule aliyefufuka.Paulo alitoa picha ya kifungo hicho cha karibu sana na kukilinganisha na uhusiano wa ndoa;"Naliwaposea Mume mmoja,yaani Kristo,ili niwalete ninyi kwake mkiwa bikira safi" 2 wakoritho 11:2.
Kulingana na maneno ya Paulo, Kanisa la Kikristo ni mwanamke safi, ni bibi-arusi wa Kristo,ishara inayofaa kabisa kwa kanisa lake alipendalo.Katika Agano la kale mithali iyo hiyo inatumika kuielezea Israeli,yaani,wateule wa Mungu.Mungu aliwaambia Israeli: wewe kama bibi-arusi ulinipenda mimi'(Yeremia 2:2) "Mimi ni mume wenu"(Yeremia 3:14).
sehemu ya pili ya somo hili tutaangalia kitabu cha Ufunuo kinavyozungumza juu ya kanisa kama mwanamke.