Thursday, June 12, 2014

YESU ANAVYOLITAZAMA KANISA LAKE-sehemu ya kwanza

Kabla Yesu hajawaambia wanafunzi wake mtazamo wake juu ya kanisa alijaribu kuwauliza wao wanamtazamaje.  “Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa nani?” (Mathayo 16:13). 
 Na Yesu akapewa majibu. Majibu tofauti-tofauti kutoka mitazamo yao tofauti-tofauti. Kulikuwa na hao waliosema Yesu ni Yohana Mbatizaji; wengine walisema Yesu ni Eliya; Yesu ni Yeremia; Yesu ni mmojawapo wa manabii. Bila shaka Yesu alihuzunishwa na majibu yao. Kwa sababu Yesu alikuwa zaidi ya Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia, au nabii. 
Baadaye, Petro akamtuliza Yesu kwa jibu sahii: “Wewe ndiwe Kristo (Masihi-Mkombozi aliyetumwa na Mungu), Mwana wa Mungu aliye hai?” Haleluya! Hapo, hapo Yesu akampongeza akimwambia, una bahati, huo sio mtazamo wa kibinadamu, “mwili na damu havikufunulia hili, bali baba yangu aliye mbinguni”(fungu la 18). Kwa lugha nyingine, Petro kwa kuwa unanitazama kwa macho ya imani kama mwana wa Mungu na mkombozi, subiri nitakueleza watu wenye imani kama yako ninavyowatazama. Kaa chini basi nilitambulishe kanisa langu kwako kama ninavyolitazama. Yesu anapompongeza Petro kwa kumtambua; hamwiti Petro, isipokuwa anamwita Simoni Baryona, hilo ndilo jina lake alilopewa na wazazi wake. Petro ni jina la kupewa-“jina la ubatizo” (Yoh 1:42). Petro  lina maana katika kiyunani kama mwamba. Na katika kiaramaki (lugha mama ya Yesu na Petro) mwamba huitwa kefa. Kwa kuwa Yesu alikuwa anaongea na Petro kwa kiaramaki bila shaka Yesu aliongea hivi: “Wewe ndiwe Kefa (mwamba) na juu ya kefa (mwamba)  nitalijenga kanisa langu”
Ni kweli Simoni mwana wa Yona ni sawa na wanadamu wengine. Lakini hapa Simon ameonesha ukefa, upetro, umwamba. Na ninyi ni mashahidi, wengi wamechagua kuyumbishwa na upepo wa maoni ya watu kunihusu mimi. Wengi wameniona kama Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia, na kama nabii tuu. Lakini hapa Simon amejibu kama Petro (jiwe); amekataa kusogezwa na maoni ya wengi, kama mwamba usivyosukumwa na upepo. Petro ni muumini wa kwanza kunikiri mimi kama Mwana wa Mungu. Imani ya Petro kwangu kama Masihi na Mwana wa Mungu ni mwamba imara na salama ambao juu yake nitalijenga kanisa langu. 
 Na hapo labda unataka kujua, Je! Yesu alijenga kanisa lake juu ya imani ya Petro? Ni kweli kanisa leo linasimama juu ya imani ya mtume Petro:
·Katika mathayo 16:16 Petro ni wa kwanza kumkiri Yesu kama Mwana wa Mungu.
·Katika Matendo sura ya 2 Petro ndio wa kwanza kumtangaza Yesu kama Masihi na Mwana wa Mungu kwa Wayahudi
·Na katika Matendo sura ya 10 tunamkuta Petro tena kama mhubri wa kwanza wa Yesu kama Masihi na Mwana wa Mungu kwa Wamataifa.

Kwa kifupi wayahudi kwa wamataifa wanaikiri imaini ile ile ya Petro kwa Yesu. Kama Petro wakristo leo: 
·Tunaamini Yesu ni Masihi na Mwana wa Mungu hata kama wengine hawaamini hivyo.
·Leo hii tunaamini Yesu ni Masihi aliyetumwa na Mungu kutukomboa hata kama wengine hawamuoni hivyo. 
·Tunamwona Yesu kama Mungu mwenye nguvu hata kama wengine wanamwona ni mwana wa Mariam tu. 

Na ni imani hii ndio inayotufanya tusalie salama kama jengo lililosimama mwambani. Imani hii na mtazamo huu ndio mwamba. Msingi wa maoni ya wengi kuhusu Yesu kama nabii tu, mwalimu tu hautufai kusimamisha imani yetu juu yake. Misingi hiyo haitulii kama mchanga wa mwambao. Leo ipo kesho imechukuliwa na maji. Tunaposongwa na mitazamo tofauti tofauti juu ya Yesu ni muhimu kutoyumbishwa kama Petro. Na tukisimamia katika imani ya Petro tuko salama.

Hivyo, mbele ya macho ya Yesu kanisa la Mungu ni Jengo linalosimama juu ya mwamba wa imani. Ndivyo linavyosimama mbele ya macho ya Yesu.

ENDELEA KUJIFUNZA MTAZAMO WA YESU KWA KUNDILAKE  DUNIANI. ROHO WA BWANA AWE PAMOJA NAWE.AMINA

No comments:

Post a Comment