Friday, June 13, 2014

YESU ANAVYOLITAZAMA KANISA LAKE-sehemu ya pili

Kanisa(waumini wanaokiri Imani ya Petro kwa Yesu) wamepewa funguo za ufalme wa mbinguni.
angalia nami mathayo 16:19: “Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni”. Kwa maneno mengine Yesu anasema, "Kefa nitakupa  wewe funguo [wewe kefa ambaye hukutetereka kunikiri mimi kama Masihi na Mwana wa Mungu]. Wewe ni mshika funguo, mlinzi katika malango ya ufalme.” Unaweza kufunga na kufungua, kuruhusu na kuzuia, wewe ni mlinzi. 
Lakini Kefa au waumini wanaokiri imani ya Kefa ni walinzi wa namna gani mlangoni pa ufalme?  

Kabla hatujaelewa maana ya ufunguo: unakumbuka maneno ya Yesu kwa walimu wa dini katika Luka 11:52? Yesu alisema, “Ole wenu, enyi wana-sheria, kwa kuwa mmeuondoa ufunguo wa maarifa; wenyewe hamkuingia, na wale waliokuwa wakiingia mmewazuia.” Mahali pengine Yesu anawalaumu Mafarisayo (washika dini) kwa kosa hilo hilo (Math 23:13). Mara zote hizo funguo zinasimama badala ya maarifa na ujuzi waliopewa. Wana-sheria na Mafarisayo walikuwa na ujuzi wa maandiko ambao ungeweza kuwanufaisha wao na wengine. Lakini hawakutumia maarifa hayo ipasavyo.

Na kwa Petro na waumini wote, ujuzi na maarifa ya ufalme umetolewa.
Petro na waumini tumefunuliwa na Baba wa mbinguni kumwona Yesu kama Masihi na Mwana wa Mungu. Ufunuo huo ni ufunguo langoni mwa ufalme. Injili ya Yesu yaweza kuwafungulia malango ya ufalme wote wanaoipokea na kuwafungia malango hayo hayo wanapoikataa. Petro na sisi wakristo tumepewa funguo nyeti. 

Lakini mwenzetu Petro alizitumiaje funguo zake? Historia takatifu imerekodi kwa ufasaha jinsi mtume Petro alivyotumia maarifa ya kumjua Yesu masihi, kwa mfano: 
·   Petro alizitumia funguo hizo siku ya Pentekoste alipowaonesha wayahudi  kuwa Yesu ni Masihi na Mwana wa Mungu aliye hai. Akawaambia, “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi” (Mdo 2:38). Na siku ile wengi kwa kumsikia Petro na kukubali  ujumbe wake walifunguliwa malango ya ufalme—tunaambiwa maelfu.
·  Mara nyingine Petro alimfungulia malango ya ufalme Kornelio na nyumba yake na wote wakaingia (Mdo 10)
· Mara nyingine Petro  akiwa na Yohana alimfungulia kiwete langoni mwa hekalu naye akapokea uponyaji
·  Mara nyingine Petro na Yohana wakawafungulia wasamaria nao wakapokea Roho Mtakatifu
·Lakini mara nyingine Petro alimfungia Anania na Safira na hawakuingia katika ufalme

Funguo alizopewa Petro ndizo tulizopewa. Tumepewa kuwafungulia watu wamjue Yesu kama Mkombozi nao wafunguliwe. Na kama kila mmoja wetu aliyepewa funguo hizi atazitumia wangapi wangepokea msamaha wa dhambi, wangapi wangefunguliwa na utumwa wa dhambi, wangapi wangepokea uponyaji. Yesu analitambulisha Kanisa kama walinzi katika malango ya ufalme. Ni bahati kuu kiasi gani lakini ni wajibu mzito namna gani kumiliki funguo za lango kuu la uzima?



No comments:

Post a Comment